Katika juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kubadilishana uzoefu katika sekta ya elimu, timu ya wataalamu wa elimu kutoka Zanzibar imeendelea na ziara yao ya siku tano ya mafunzo mkoani Katavi kwa kutembelea Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe Februari 04, 2026.

Ziara hiyo imelenga kujifunza na kushirikishana mbinu bora za utekelezaji wa sera na mipango ya elimu, hususan katika maeneo ya elimu ya awali, msingi na sekondari, pamoja na matumizi ya teknolojia na rasilimali rafiki kwa mazingira.

Akiwa wilayani Mpimbwe, ujumbe huo umetembelea Shule ya Sekondari Mizengo Pinda ambako umejifunza kuhusu matumizi ya mfumo wa nishati safi ya kupikia, hatua inayolenga kupunguza matumizi ya kuni na mkaa pamoja na kulinda mazingira. Aidha, wataalamu hao walipata fursa ya kutembelea darasa la awali pamoja na Shule ya Msingi Ibuka, ambapo walijionea mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji pamoja na juhudi zinazochukuliwa kuboresha elimu ya msingi.

Ziara hiyo pia ilihusisha kutembelea chemchemi ya maji ya moto, kama kivutio cha asili na rasilimali ya kipekee ya Halmashauri hiyo, pamoja na kiwanda cha kuchakata mchele, ambapo ujumbe huo ulipata maelezo kuhusu mchango wa sekta ya kilimo na viwanda vidogo katika kuinua uchumi wa wananchi na kusaidia maendeleo ya elimu kupitia mapato ya ndani.

Kwa ujumla, ziara hiyo imeelezwa kuwa na manufaa makubwa kwa pande zote mbili, ambapo wataalamu kutoka Zanzibar wamepata uzoefu wa vitendo, huku Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe ikiendelea kujitangaza kama kitovu cha ubunifu na ushirikiano katika sekta ya elimu na maendeleo ya jamii.
Mpanda-Katavi (Mkoani Area)
Sanduku la Barua: Box 235, Mpanda -Katavi
simu: 025-2957108
Mobile:
Barua pepe: ras.katavi@tamisemi.go.tz
Copyright@2017 Katavi Rs. All right reserved