Kikao cha tathmini ya maendeleo ya sekta ya viwanda, biashara na uwekezaji kwa kipindi cha miaka mitano kimefanyika leo Juni 26,2025 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi, kikihusisha maafisa biashara kutoka Halmashauri zote za mkoa pamoja na wadau wa sekta ya viwanda na biashara. Kikao hicho kimekuwa jukwaa muhimu la kupima hali ya biashara na uwekezaji, pamoja na kuweka mikakati ya kuboresha mazingira ya uchumi wa mkoa.
Katibu Tawala wa Mkoa, Bw. Albert Msovela, ameongoza kikao hicho na kubainisha kuwa bado kuna changamoto kubwa ya upatikanaji wa elimu kwa wafanyabiashara, hali inayowapelekea wengi wao kuendesha shughuli bila kuwa na leseni halali. Amesisitiza kuwa ni wajibu wa maafisa biashara kuhakikisha wanawafikia wafanyabiashara, kuwapatia elimu stahiki na kuwatengenezea mazingira rafiki ya kufanyia biashara.
Ameelekeza pia kufuatiliwa kwa karibu mikataba inayotolewa na wawekezaji, hasa kwenye sekta ya madini, ili kuhakikisha haibebi masharti kandamizi kwa wazawa. Amesema ni muhimu kulinda haki za wafanyakazi wa ndani katika maeneo yote ya uwekezaji.
Ametoa pongezi kwa TRA na Wakala wa Madini kwa juhudi zao za kuhakikisha ukusanyaji wa mapato unafanyika kwa uwazi na kwa kutoa taarifa za kila mwezi za utendaji wao. Amezitaka taasisi nyingine za umma kuiga mfano huo ili kuongeza uwajibikaji na kuimarisha huduma kwa wananchi.
Ameeleza pia kuwa maeneo mengi ya uwekezaji yamevamiwa, na amewataka maafisa biashara kuchukua hatua za haraka kukabiliana na hali hiyo kabla haijathiri zaidi mwelekeo wa maendeleo ya mkoa. Aidha, ameagiza mabaraza ya biashara kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na kuhakikisha vikao vinafanyika mara kwa mara kama ilivyoainishwa kwenye miongozo.
Ameomba Katibu Tawala Msaidizi, anayeshughulikia masuala ya viwanda na biashara, Bw. Florence Chrisant, kuratibu kwa karibu utoaji wa elimu endelevu kwa wafanyabiashara pamoja na kusimamia matumizi sahihi ya vipimo ili kuhakikisha biashara zinafanyika kwa haki na kwa kuzingatia viwango vinavyokubalika.
Mpanda-Katavi (Mkoani Area)
Postal Address: Box 235, Mpanda -Katavi
Telephone: 025-2957108
Mobile:
Email: ras.katavi@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Katavi RS . All rights reserved.