Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Profesa Ibrahim Juma, ameongoza kikao muhimu kati ya Watumishi wa Mahakama na Wadau wa Mahakama mkoani Katavi, ambapo amesisitiza uadilifu miongoni mwa watendaji wa Mahakama pamoja na mchango wa wadau katika kuimarisha huduma za utoaji haki nchini.
Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika Mei 28, 2025 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe. Profesa Juma amesema kuwa uadilifu kwa watumishi wa Mahakama ni nguzo kuu ya kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa wakati, kwa usawa na bila upendeleo. Ameeleza kuwa Mahakama haiwezi kutimiza wajibu wake ipasavyo pasipo misingi imara ya maadili, weledi na uwajibikaji.
Aidha, Jaji Mkuu amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kutoka kwa taasisi mbalimbali za umma katika kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050. Amebainisha kuwa mafanikio ya dira hiyo yanahitaji mshikamano wa kitaifa pamoja na kujenga mfumo wa haki unaoendana na mabadiliko ya kijamii, kiuchumi na kiteknolojia.
Kwa upande wake, Jaji Kiongozi na Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. Mustapher Siyani, amewasihi viongozi wa umma na wananchi kwa ujumla kuepuka kujadili mashauri yanayoendelea mahakamani, akieleza kuwa hali hiyo huathiri mwenendo wa kesi na hupunguza imani ya wananchi kwa mfumo wa utoaji haki
Mhe. Siyani pia amewahamasisha wananchi wa Katavi kuchangamkia fursa za ajira kama madalali na wasambaza nyaraka wa Mahakama, akibainisha kuwa kwa sasa mkoa wa Katavi una dalali mmoja pekee kati ya 118 waliopo nchi nzima.
Akihitimisha kikao hicho, Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe. Mwanamvua Mrindoko, amemshukuru Jaji Mkuu kwa kufanya ziara hiyo mkoani Katavi na ameahidi ushirikiano wa karibu na Mahakama katika kuhakikisha haki inatolewa kwa mujibu wa sheria na inawafikia wananchi wote.
RC Mrindoko ameahidi kuwa Katavi itakuwa kinara wa ujenzi wa maboma ya Mahakama, na ameukaribisha uongozi wa Mahakama kufanya shughuli za kitaifa na kikanda mkoani Katavi, akitaja vivutio vya mbuga ya Katavi, misitu ya asili na fursa ya biashara ya kaboni kama sehemu ya utajiri wa mkoa.
Mpanda-Katavi (Mkoani Area)
Postal Address: Box 235, Mpanda -Katavi
Telephone: 025-2957108
Mobile:
Email: ras.katavi@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Katavi RS . All rights reserved.